Saturday 28 03 2020 Daily Mass - a podcast by St Joseph Cafasso Kingongo Parish

from 2020-03-28T09:41:20

:: ::

MASOMO YA MISA, MACHI 28, 2020


JUMAMOSI: JUMA LA 4 LA KWARESIMA




SOMO 1


Yer. 11:18-20




Bwana akanijulisha haya, nami nikayajua; ndipo uliponionyesha matendo yao. Lakini mimi nalikuwa kama mwana-kondoo mpole, achukuliwaye kwenda kuchinjwa; wala sikujua ya kuwa wamefanya mashauri kinyume changu, wakisema, Na tuuharibu mti pamoja na matunda yake, na tumkatilie mbali atoke katika nchi ya walio hai, ili jina lake lisikumbukwe tena.


Lakini, Ee Bwana wa majeshi, uhukumuye haki ujaribuye viuno na moyo, nijalie kuona kisasi chako juu yao; kwa maana nimekufunulia wewe neno langu.




Neno la Bwana… Tumshukuru Bwana.




WIMBO WA KATIKATI


Zab. 7:1-2, 8-12 (K) 1




(K) Bwana, Mungu wangu, nimekukimbilia Wewe.




Bwana, Mungu wangu, nimekukimbilia Wewe,


Uniokoe na wote wanaonifuatia, uniponye.


Asije akaipapura nafsi yangu kama samba,


Akiivunja-vunja pasipokuwa na wa kuponya. (K)




Bwana, unihukumu mimi,


Kwa kadiri ya haki yangu,


Sawasawa na unyofu nilio nao.


Ubaya wao wasio haki na ukome,


Lakini umthibitishe mwenye haki. (K)




Ngao yangu ina Mungu,


Awaokoaye wanyofu wa moyo.


Mungu ni mwamuzi mwenye haki,


Naam, Mungu aghadhibikaye kila siku. (K)




SHANGILIO


Lk. 15:18




Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia: Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako.




INJILI


Yn. 7:40-52




Wengine katika mkutano walipoyasikia maneno ya Yesu, walisema, Hakika huyu ndiye nabii yule. Wengine walisema, Huyu ndiye Kristo. Wengine wakasema, Je! Kristo atoka Galilaya? Andiko halikusema ya kwamba Kristo atoka katika uzao wa Daudi, na kutoka Bethlehemu, mji ule alioukaa Daudi? Basi kukaingia matengano katika mkutano kwa ajili yake. Baadhi yao wakataka kumkamata, alkini hakuna mtu aliyenyosha mikono yake ili kumshika.


Basi wale watumishi wakawaendea wakuu wa makuhani na Mafarisayo. Nao wakawaambia, Mbona hamkumleta? Wale watumishi wakajibu, Hajanena kamwe mtu yeyote kama huyu anavyonena. Basi Mafarisayo wakawajibu, Je! Ninyi nanyi mmedanganyika? Ni nani katika wakuu amwaminiye, au katika Mafarisayo? Lakini makutano hawa wasioifahamu torati wamelaaniwa.


Akawaambia Nikodemo, (naye ni yule aliyemwendea zamani, maana ni mmoja wao), Je! Torati yetu humhukumu mtu kabla ya kumsikia kwanza, na kujua atendavyo? Wakajibu, wakamwambia, Je! Wewe nawe umetoka Galilaya! Tafuta, ukaone ya kuwa kutoka Galilaya hakutokea nabii.




Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Further episodes of St. Joseph Cafasso King'ong'o Parish

Further podcasts by St Joseph Cafasso King'ong'o Parish

Website of St Joseph Cafasso King'ong'o Parish